Karatu
Watalii wanaokwenda kwenye nyanda za kaskazini kuelekea mbuga ya Serengetina Bonde la Ngorongoro lazima watapitia mji wa Karatu na chini ya “huruma” ya kilele cha Ol Deani. Ukimaliza tu kupanda mwinuko wa Manyara unakutana na hali ya misitu minene ya kijani na hatimaye unaingia kwenye nyanda za Karatu. Masalia ya volkano ya Ol Deani hutengeneza miteremko inayoongeza uzuri wa mandhari ambayo ni kivutio maalum kwenye eneo hilo.
Katika siku za nyuma, maeneo yanayozunguka mji wa Karatu na Ol Deani yalikuwa muhimu sana kwa utawala wa kikoloni wa Wajerumani. Hali ya hewa ya ubaridi baridi katika eneo hili yenye milima iliyosheheni mimea na mandhari ya kupendeza iliwavutia sana walowezi na wakulima wakubwa. Mashamba makubwa yameenea katika miteremko yote ya milima ya volkano na kuzunguka mji wa Karatu.
Wakati huo, kahawa ilikuwa ni zao kuu la biashara ya nje na mashamba makubwa machache yaliyosalia huko Karatu yako mikononi mwa watu binasfi bado yanazalisha zao hili. Mji wa Karatu una mandhari nzuri katika nyanda hizi za kaskazini na kituo kikuu kwa watalii wanaoelekea Bonde la Ngorongoro.



Je ulikuwa wajua?


