Mahali ilipo
Tanzania – mahali ilipo (Location)
Tanzania ipo katika eneo la Afrika Mashariki kwenye nyuzi 6 00S (kusini) na 35 00E (mashariki) ikipakana na Kenya na Uganda upande wa kaskazini, Rwanda, Burundi na Jamhuri ya Watu wa Congo upande wa magharibi, Zambia na Malawi kwa upande wa kusini-magharibi na Msumbiji, kusini. Upande wa mashariki inapakana na pwani ya Bahari ya Hindi wenye urefu wa kilomita 1,424. Nchi hii ina jumla ya eneo la kilometa za mraba 945,087 zikijumuisha visiwa vya Unguja, Pemba na Mafia. Kati ya hizo kilometa za mraba 886,037 ni nchi kavu.
Urefu wa mipaka na nchi jirani ni kama ifuatavyo: Burundi – kilometa 451, DRC km 676, Kenya km 769, Malawi km 475, Msmbiji km 756, Uganda km 396 na Zambia km 338.
Tanzania ina ukanda wa pwani wenye urefu wa kilometa 1,424. Kufuatana na sheria ya kimataifa, Jamhuri ya Muungano ya Tanzania inamiliki kilometa 12 za sehemu ya bahari (territorial waters) na kilometa nyingine 200 kama eneo lake la kuendesha shughuli za kiuchumi (Exclusive Economic Zone – EEZ).
Hali ya hewa, nchini Tanzania inatofautiana kulingana na mazingira. Sehemu ya pwani ina hali ya joto (kitropiki) na sehemu ya nyanda za juu kuna ubaridi kiasi (temperate).
Hali ya nchi ni tambarare katika ukanda wa pwani na miinuko katikati mwa nchi, ambapo kaskazini na kusini imetawaliwa na milima milima.
Mwinuko wa nchi unaanzia kwenye usawa wa Bahari ya Hindi (0 m) hadi kwenye kilele cha Mlima Kilimanjaro (5895 m). Maliasili ya Tanzania ni pamoja na wanyamapori, misitu, madini (maarufu: almasi, dhahabu, tanzanite, chuma, mkaa wa mawe, gesi asilia) na viumbe wa baharini.
Matumizi ya ardhi: Tanzania inatumia 4.23% tu ya ardhi yake kwa ajili ya kilimo na kati ya hizo 1.16% huzalisha mazao ya kudumu. Eneo linalotumika kwa ajili ya kilimo cha umwagiliaji ni kilometa za mraba 1,840.
Dokeza za kijiografia: Mlima Kilimanjaro ni mrefu kuliko yote katika bara la Afrika. Ziwa Victoria ni la pili kwa ukubwa duniani na Ziwa Tanganyika ni la pili kwa kuwa kina kirefu duniani. Ziwa Nyasa ambalo liko kusini magharibi mwa Tanzania linaaminika kuwa lenye mawimbi makubwa (dhoruba) kuliko maziwa yote duniani.



Je ulikuwa wajua?


